JINA LA SIMULIZI............................LISA
AUTHOR...........................JOMBA WAJO
SPONSORED BY......SIMULIZI ZA DULLY
WHATSAPP..........................0628924768
SEHEMU YA................................248-249

Sura ya: 248

Usiku, Shangazi Yasine alikuja na chakula cha jioni. Hisia tata ilijidhihirisha katika moyo wa Alvin alipoona bendeji kuzunguka kichwa cha Aunty Yasmine. “Unapaswa kupumzika nyumbani. Nitamwambia Hans atafute mlezi mwingine…”
“Si sawa, Bwana Mkubwa. Kukuona ukiwa katika hali hii inanitia wasiwasi.”
Alvin akatenganisha midomo yake kutaka kusema kitu lakini akabadilisha mawazo yake. Akifikiri kwamba Aunty Yasmini angeogopa. Aliishia tu kusema kwa upole, “Pole…”
“Sijambo, lakini Bibi Mdogo hajakuelewa,” alisema. “Nyinyi mligombana kimakosa usiku huo, na sikupata nafasi ya kukueleza. Kweli, Bi. Kimaro hakumpiga Maurine bila sababu. Alikuja nyumbani akakuona wewe na Maurine mmelala kwenye kitanda kimoja. Kama ningekuwa mimi, nisingeelewa pia.”
"Nini?" Alvin alimtazama mwanamke huyo kwa macho yake meusi. "Kwanini Maurine alikuwa kitandani kwangu?"
Alijibu kwa unyonge, “Ulirudia usiku siku hiyo. Ulimshika mkono wake mara tu alipojitokeza, hata baada ya kukupeleka kitandani, ulisisitiza abaki na wewe. Bwana Mkubwa … Jnaogopa kusema lakini ulimkosea Bibi Mdogo!”
Alvin alichanganyikiwa. Ina maana alimshika mkono Maurine na kwenda naye chumbani kwake? Hakuwa na kumbukumbu yake hata kidogo.
Kisha akaendelea. “Nilitaka kumzuia Bi. Kimaro usiku ule baada ya kurudi, lakini aliwahi kukimbilia ghorofani na kuwakuta katika hali hiyo. Alilalamika na kuanza kugombana na MAurine lakini ukamuona kama mkorofi. Ulimfungia hata kwenye chumba cha upweke baada ya hapo. Naamini alishtuka sana.”
“Mimi… nilimfungia ndani ya chumba?” Hilo nalo lilimshangaza. Hakukumbuka hata kama waligombana.
"Hiyo ni kweli. Bi. Kimaro alipiga kelele za kuomba msaada usiku mzima. Alivunjika moyo sana. Alishangaa kwamba ulimfungia ndani ya chumba cha upweke baada ya kile wanafamilia wako walimfanyia mara ya mwisho.”
Hisia nzito katika kifua chake ilimsababishia maumivu makali. Alikuwa amefanya nini? Kichwa chake kilianza kumuuma tena.
Akiwa amechanganyikiwa, Aunty Yasmine haraka akachukua mto na kuuweka nyuma ya shingo yake. Hata hivyo, maumivu ya kutoboa moyo yalimzuia asilale usiku wote huo.
•••
Asubuhi. Lisa aliingia ofisini kwake. Hans alikuwa akimngoja nje ya ofisi yake kwa muda mrefu. "Bibi mdogo, haya ni majibu ya vipimo vya DNA kati ya Melanie na Bw. Joel Ngosha ambayo ulitaka nishughulikie hapo awali."
Hilo lilimshangaza Lisa. Alikuwa amekosana na Alvin, na hivyo hakutarajia msaidizi wake angeendelea kumsaidia.
"Asante." Alipokea hati kabla ya kusema, “Hii itakuwa mara ya mwisho kuomba msaada wako. Tafadhali acha kuniita Bibi Mdogo baada ya hapa. Huyo si mimi tena.”
"Wewe ni bosi wangu mradi tu umeolewa na Bwana Mkubwa." Akakunja uso kwa wasiwasi. “Kwa kweli, Bwana Kimaro anajali sana kuhusu wewe. Juzi usiku baada ya nyie kutoka kwenye baa, alizimia na hakurudiwa na fahamu hadi jana. Hayupo vizuri kwa sasa. Jana usiku, yeye…”
“Unapaswa kumtafuta Maurine. Au tembelea kaburi la mpenzi wake wa zamani.” Kuzungumza juu ya Alvin kuliharibu hisia zake. Watu wengi waliokuwa karibu na Alvin waliendelea kumwambia kwamba anamjali, kwamba hali yake ingezidi kuwa mbaya bila yeye. Aliwaamini. Hata alijishusha chini ili kuwafurahisha watu wa familia ya Kimaro. Lakini, alipata nini mwishowe? Unyonge na uongo.
“Bwana Mkubwa hampendi Maurine…”
“Hans, acha. Mimi si shirika la kutoa misaada.” Alimkatiza bila kusita, na chuki machoni mwake ilielezea kila kitu.
Hans alishindwa cha kusema. Alishusha pumzi baada ya kuingia kwenye lifti. Laiti angejua hivyo ndivyo mambo yatakavyokuwa, angemshawishi Alvin asimuajiri Maurine hapo mwanzo.

Lisa alivumilia hisia ya kichefuchefu hadi akakimbilia kwenye chumba cha kunawia ili kutapika. Alikuwa amekunywa sana jana yake hadi tumbo likaanza kumsumbua. Baada ya hapo, aliendelea kusoma hati iliyokuwa mkononi mwake.
'Haihusiani' ilionekana mbele ya macho yake kwa maneno mekundu na ya ujasiri. Hiyo ilimshangaza sana Lisa. Melanie hakuwa binti wa Joel. Hata hivyo, Joel alimtelekeza mama yake ili amuoe Nina zamani kwa sababu Nina alikuwa na ujauzito wa Melanie.

Kwa maneno mengine, Nina alikuwa amemdanganya Joel zaidi ya miaka ishirini iliyopita. Lisa akaweka hati hiyo kwa uangalifu. Hizi zilikuwa habari za kushtua lakini wakati wa kuziweka hadharani ulikuwa bado.
Akiwa anawaza hayo tu, Daktari Angelo akampigia simu. “Bi Jones, sehemu niliyokuwa nakaa jana usiku iliteketea kwa moto ghafla. Kwa bahati nzuri, ulinikumbusha kuwa ninaweza kuwa katika hatari muda wote, kwa hivyo nimekuwa nikitoka kwa siri kupitia mlango wa nyuma baada ya kufika nyumbani. Utabiri wako ulikuwa sahihi sana."
“Hilo ni la kushukuru Mungu. Tafadhali mwagize msaidizi wako atangaze kwamba ulikufa kwa moto. Kwa sasa, tafadhali endelea kumhudumia baba yangu kwa siri.”
Lisa alitabiri kuwa Damien angeweza kumdhuru daktari huyo maarufu. Kwa bahati nzuri, Daktari alizingatia ushauri wake na akaokoka. Damien na wengine lazima wangeamini kuwa Daktari Angelo alikuwa amekufa kwa muda huo.
•••
Katika makazi ya familia ya Ngosha, Nina alitabasamu kwa furaha baada ya taarifa za kifo cha daktari. “Kwa kweli ni habari njema. Joel hawezi kurejewa na fahamu hivi karibuni baada ya kifo cha Dokta Angelo. Lisa ni mjinga sana kuendelea kuhangaika na baba yake. Lazima atakuwa akilia na moyo wake sasa hivi.”
Melanie alichanganyikiwa. “Mama unamaanisha nani? Baba yangu?"
"Ndio, baba yako yuko njiani kuja hapa ili nyinyi wawili mkutane rasmi. Tutalazimika kumtegemea katika siku zijazo." Nina alimpigapiga bintiye kichwani. Ijapokuwa alimdharau mwanaume huyo miaka yote, ilimbidi akubali kwamba aliweza kumpa kile anachotaka, tofauti na Joel ambaye hakuacha kumfikiria Sheryl.
Melanie alimtazama kwa macho ya kutarajia. Dakika chache baadaye, mwanamume mmoja aliingia akisukumwa kwa kiti cha magurudumu. Melanie alipigwa na butwaa kumwona, lakini hatimaye, alifikiri kwamba yote yalikuwa ya maana. Si ajabu alifanana na Joel ingawa hakuwa baba yake halisi. Isitoshe, Damien alikuwa amemdekeza tangu alipokuwa mtoto. Haijalishi angefanya nini, angemsaidia kila wakati.
“Melanie, njoo huku. Mimi ni baba yako.” Damien alimwashiria.
“Bam’dogo Damien… ni wewe?” Alitembea kuelekea kwake kwa kusitasita.
Alikunja uso, na Nina akaeleza hali hiyo haraka. “Kwa kweli, baba yako amekuwa akinipenda tangu miaka ishirini au zaidi iliyopita. Lakini sikujua vizuri zaidi na kuweka matumaini yangu yote kwa Joel. Kabla Joel hajanioa, mimi na baba yako tulikuwa tayari tumekuweka tumboni mwangu. Baada ya hapo, niliwaambia kuwa mtoto wangu ni wa Joel ili anioe. Miaka yote, Damien amekuwa akitutunza. Bila yeye, Lisa angekuwa na udhibiti kamili wa Ngosha Corporation kwa sasa.”
“Ni kweli bam’dogo?” Melanie alikuwa katikati ya mshangao.
“Acha kuniita bam’dogo Melanie. Niite baba badala yake.” Alishika mikono ya Melanie. "Nitakupa kilicho bora zaidi."
“Asante, Baba.” Alimzungushia mikono yake shingoni. Damien alimjali sana kuliko Joel. “Baba, namchukia Lisa. Nataka afe.”
Nitamfanya yeyote anayemdhulumu binti yangu alipe kwa matendo yake. Lakini kipaumbele kwa sasa ni kuharakisha harusi yako na familia ya Campos,” alisema. "Familia ya Kimaro haitakuwa na nafasi katika jiji hili mara tu familia za Ngosha na Campos zitakapoungana tena."

Sura ya: 249

Melanie alikuwa ameduwaa. “Baba, unapanga…”
“Nataka uwe mwanamke mashuhuri wa Nairobi. Utatafutwa na kuonewa wivu na kila mtu.” Macho ya Damien yalijaa kujiamini. "Siku hiyo itakuja hivi karibuni."
Melanie aliwazia tukio hilo, na mwili wake ukatetemeka kwa msisimko.
•••
Saa tano usiku, Lisa alirudi nyumbani baada ya kutoka kutazama sinema. Alipofungua mlango, alihisi kuwa kuna kitu hakiko sawa. Harufu ya waridi sebuleni ilikuwa kali sana. Kulikuwa pia na jozi ya viatu vya kiume kwenye mlango.
Moyo wake uliruka mapigo. Akawasha taa. Maua mengi mekundu yalikuwa yamepangwa katika umbo la moyo katikati ya sebule. Alvin alikaa kwenye sofa la kitambaa huku akiwa amevalia fulana nyeusi iliyomechishwa na suruali nyeusi ya jeans. Hata nywele zake zilikatwa katika mtindo wa kiduku, ambao kwa kipindi hicho ulikuwa ukivuma katika tasnia ya burudani. Mavazi yake pamoja na sura yake, vilimfanya aonekane tofauti kabisa na alivyozoeleka.
Lisa karibu hakuweza kumtambua. Huyo alikuwa Alvin? Kwanini alionekana hivyo siku hiyo? Alionekana kama mvulana aliyetoka tu shuleni, ambaye alikuwa akimtongoza mpenzi wake kwa mara ya kwanza.
“Ninaonekana vizuri?” Alvin alimuona Lisa akimshangaa, akafunua midomo yake kuachia tabasamu zito. Ilionekana kama kidokezo cha siri cha Chester kilikuwa kimefanya kazi.
Wanawake huwapenda wanaume ambao hujua namna ya kubadilisha hisia zao muda wowote. Mwanamume ambaye anaweza kumchukiza na kumwonyesha mapenzi. Mwanamume anayeweza kumliza na kumfanya acheke. Mwanamume anayeweza kumhudhunisha na kumfurahisha. mwanaume anayeweza kucheza vizuri na hisia za mwanamke, hatakosa penzi la mwanamke ampendaye.
Ingawa hakuwahi kufanya hivi hapo awali, alikuwa tayari kubadilisha mtazamo wake mara moja moja kwa ajili ya Lisa tu.
Lisa alimsoma kwa umakini na kukunja uso. "Maurine anakutunza au anakuharibu ubongo?"
“Una wasiwasi na mimi?” Alvin alizidi kutabasamu. "Ninajisikia vizuri zaidi baada ya kukuona."
"Hapana, umekata nywele zako kwa mtindo huu wa kitoto na hata ukaingia kwenye nyumba ya mtu mwingine na kujaza rundo la takataka. Hii haimaanishi kwamba umekuwa mgonjwa zaidi?” Lisa akacheka kwa kejeli. “Nadhani vitu hivi hujavileta mahali sahihi. Ungepeleka mbele ya kaburi la Sara.”
Alvin alijikaza. Alikuwa ameishi kwa miaka 30, lakini ilikuwa ni mara ya kwanza kuhisi kana kwamba alikuwa anapigwa kofi usoni la mwanamke.
“Lazima uwe mwendawazimu. Unawezaje kujaza takataka zote hizi kwenye nyumba yangu?" Lisa aliumwa na kichwa kwa kuangalia maua yale. Alitumia siku nzima kusafisha nyumba hii mpya, lakini alikuta uchafu mwingine umetapakaa nyumba nzima.
Alvin alijisikia vibaya ghafla kutokana na kejeli za maneno ya Lisa. Alihisi moyo wake unakuwa mweusi kama umepakwa masinzi. Alikuwa ametumia muda mwingi kupanga maua yale, na mikono yake ilichomwa na miiba kila mahali. Lakini juhudi yake ilionekana kama utopolo tu kwa Lisa.
“Kwanini upo hapa?” Lisa alimtazama bila furaha. “Umeingiaje? Tafadhali ondoka mara moja, la sivyo nitakuripoti kwa polisi kwa kosa la kuvamia kwenye nyumba ya mtu bila kukaribishwa.”
“Sawa, unaweza kuendelea na kuniripoti. Nitawaonyesha polisi hiki kitu.” Alvin akatoa cheti chao cha ndoa. “Sisi bado ni mume na mke, kwa hivyo nina haki za kisheria kukaa hapa."
Lisa alikosa la kusema. Alikaribia kusahau kwamba Alvin alikuwa wakili bora zaidi nchini Kenya.
“Kwa hiyo unataka kumleta Maurine na kuwa na wanawake wawili wakimtumikia mume mmoja?” Lisa alidhihaki, "Naona huu ni utaratibu wa kawaida wa matajiri wakubwa wa hapa Nairobi ambapo mke halali na mchepuko huishi pamoja katika nyumba moja."
Alvin alisimama mara baada ya kusikia maneno yake ya kejeli. Umbo lake jembamba lilikuwa kama la mwanamitindo, lakini macho yake yalikuwa ya damu. "Nilimtaka Maurine aondoke tayari. Shangazi Yasmine aliniambia kuwa ulimpiga usiku ule kwa sababu nilikuwa nimelala kitandani na kumshika mkono Maurine. Samahani kwa kuwa sikukuelewa. Nimekuja kukuomba msamaha.”
Alvin akaanza kufafanua jambo moja baada ya jingine.

"Kuhusu Sarah Wonderland Park, ni suala lililotokea muda mrefu uliopita. Sikujua tukio la fataki la saa mbili usiku kila Ijumaa kama bado linaendelea. Siku zote ni msimamizi mkuu wa bustani hiyo ndiye ambaye alisimamia tukio hilo. Alisema fataki hizo zimekuwa kivutio cha watalii, lakini nimemwambia asitishe.”
“Kuhusu kampuni, nilikuwa bado sijakutana na wewe nilipoipa jina la Alvinarah. Hata hivyo, nitaifanya KIM International na Alvinarah ziunganishwe haraka iwezekanavyo. Baada ya hapo, hakutakuwa tena na kampuni ya Alvinarah.”
Alvin akamsogelea Lisa hatua kwa hatua, huku macho yake yakiwa yamejaa mahaba. “Lisa, rudi mpenzi. Siwezi kuwa bila wewe." Aliinamisha kichwa chake na kumbusu midomo yake kwa upendo.
Lisa alikuwa kama ameyeyukia hewani wakati huo. Hakukuwa na shaka kwamba sura, hadhi, na sauti ya Alvin ingeweza kumvutia kwa urahisi mwanamke yoyote. Hata hivyo, pumzi yake ilipokaribia kukata, Lisa alirudi kwenye fahamu zake na kupiga hatua chache nyuma. Alimtazama Alvin kwa tahadhari.
"Nimesikia hadithi zako nyingi sana. Umewahi kuniambia maneno mengi mazuri pia, lakini ulinichukuliaje? Maurine alipojitokeza kwako akili yako ikahama kabisa, ulifikiri ninamnyanyasa. Marafiki zako wote wananifikiria kama mtu mbaya ambaye ana wivu hadi kwa mtu marehemu, na ndiyo unaowasikiliza na kuwaamini. Rodney alinihakikishia kuwa Maurine hawezi kuondoka, mimi nimechoka kabisa!”
Ukimya mfupi ulipita kisha Lisa akaendelea.
"Kulikuwa na tukio na Thomas pia. Ulijua kuwa alikuwa ameoza kabisa, lakini ulimsaidia tena na tena. Mwishowe, Zigi alikuja kuniumiza kwa kisu. Hilo lilisababisha Kelvin kupoteza figo na ilinibidi kubeba hatia…”
Alvin alikodoa macho. “Kwa hiyo unafikiri kwamba Kelvin aliumia kwa sababu yangu?”
“Kumbe!” Lisa alicheka. “Kama si Kelvin, ningekuwa nimekufa. Ningekufa kwa sababu ya kaka wa mpenzi wako wa zamani." Alisema kwa kejeli na kupanda juu. Akiwa amekasirika sana, alifunga mlango na kuingia bafuni kuoga.
Baada ya kutoka kuoga, alimuona Alvin aliyetakiwa kuwa nje akiwa amejilaza kitandani kwake. Alikuwa amelala fofofo huku akikumbatia mto wake na kujifunika blanketi lake.
Lisa alikuwa karibu kupandwa wazimu. Mtu huyo aliwezaje kuingia chumbani kwake? "Alvin, ondoa wazimu wako hapa." Lisa akainua blanketi.
Alipoona Alvin hajavaa chochote chini ya blanketi, uso wake ulibadilika kwa hasira na aibu. “Mbona umevua nguo?”
Akiutazama uso wa Lisa wenye haya, midomo ya Alvin ilijipinda na kutabasamu. "Nililazimika kuvua ili kulala, bila shaka. Hukuniandalia nguo zozote za usiku pia.”
Lisa alizidi kupandwa na hasira za mshangao. Hakuwa na aibu kiasi cha kujipenyeza ndani ya nyumba yake, akaingia chumbani kwake na kulala kitandani kwake na kumlaumu kwa kutomwandalia nguo za kulalia?
“Kuwa mstaarabu na usinisumbue. Ninaweza kulala usingizi tu kwa kuvuta harufu yako. Sijalala kabisa kwa siku mbili.” Alvin alichukua blanketi na kujifunika.
Lisa alikasirika kiasi kwamba alitamani apasuke. Alijiona hana nguvu. “Alvin, unataka nini? Maurine hakutoshi sasa? Mbona bado unaning’ang’ania?”
“Tayari nimemuamuru aondoke.” Alvin akabinya midomo yake pamoja na kusema, “Ikiwa unanichukia kwa kukufungia kwenye chumbani peke yako kwa usiku mmoja, unaweza kunifungia chumbani pia.”
Lisa alifoka, “Kwanini nikufungie? mimi si mgonjwa kama wewe.”
Mgonjwa? Neno hilo lilijirudia chumbani. Uso wa Alvin ulipauka papo hapo. Alionekana kana kwamba ni mtoto. Lisa aliuma mdomo. Hakutaka kuwa na moyo dhaifu na kumuonea huruma hata kidogo.
Alvin hakusema chochote. Alinyanyuka na kutembea kwa huzuni hadi chumba kingine kabla ya kufunga milango. Lisa hakumjali na kumwacha aendelee na maigizo yake.....ITAENDELEA...

Unafikiri nini kitafuata hapo, maana simulizi inazidi kuwa tamu kila siku lakini sina budi kuhitimisha kipande hiki ila niwasihi tukutane katika episode zijazo ili kujua nini kitafuata kwenye mkasa huu wa kusisimua na kuelimisha unaokwenda kwa jina la LISA.