JINA LA SIMULIZI............................LISA

AUTHOR...........................JOMBA WAJO

SPONSORED BY......SIMULIZI ZA DULLY

WHATSAPP.........................0628924768

SEHEMU YA...............................132, 133


Sura ya 132


Jones alitetemeka upepo wa baridi ulipovuma. Kwa mara ya kwanza, hisia ya majuto ilipanda moyoni mwake. Ilikuwa wazi kuwa alikuwa na familia nzuri. Ilivunjikaje kwa muda wa miezi mitatu tu?


Siku iliyofuata, Jones alipokea simu kwamba alikuwa amefukuzwa kutoka kwenye bodi ya wakurugenzi wa Mawenzi Investments. Alikimbilia kwenye kampuni hiyo kwa hasira, lakini mlinzi wa mlangoni hakumruhusu kabisa kuingia na kumfukuzia nje. Kwa kuwa hakuwa na mahali pengine pa kwenda, Jones aliishia kulewa kwenye baa na alirudi tu nyumbani usiku wa manane.


Usiku huo, kwa ulevi alisukuma mlango wa nyumba yake kwa unyonge na hakukuwa na taa ndani, na mwanga wa mbalamwezi wa baridi ulipenya kupitia madirishani. Kulikuwa na kiti cha magurudumu katikati ya sebule, na juu yake aliketi mwanamke mzee mwenye mgongo ulioinama na nywele zilizotawanyika. Sura hiyo ilionekana ya kutisha haswa. Jones aliogopa sana hivi kwamba miguu yake ilidhoofika. Aligeuka na kujaribu kukimbia. Hata hivyo, mlango ulifungwa nyuma yake, na sebule ikawa giza.


“Mama…” Jones alipiga magoti chini kwa woga, akitetemeka kama jani lililosukumwa na upepo.


“Mwanangu, mbona unaniogopa sana?” Kiti cha magurudumu kiliteleza mbele polepole, na sauti ya mwanamke mzee ikasikika.


Jones alirudi nyuma kwa hofu. “Mama, mama, usije. Tafadhali, si mimi niliyekudhuru. Kuna mtu mbaya."


“Si wewe uliyenidhuru?” Kicheko cha kutisha cha yule kikongwe kilisikika pale sebuleni. "Ulifanya hivyo kwa ajili ya hisa na pesa. Lakini kwa nini umenidhuru? Si nilikutunza tangu ujana? Ulimwengu wa kuzimu hautaki kunikubali kwa sababu mliniondoa kabla ya siku zangu, kwa hivyo imenibidi tu kurudi kukutafuta. Mwana…”


Kiti cha magurudumu kilikuwa kikikaribia zaidi na zaidi. Jones alipiga magoti chini na kuinama kwa nguvu, machozi na vilio vikimtoka. “Mama, nilikosea. Nilikosea. Nilianza kuhangaika, lakini sikutaka kukuumiza. Ilikuwa Mama Masawe. Mama Masawe ndiye alikusogezea mto. Nenda kwake badala yake.


“Kama hukukubali, angeniua?” Mwanamke mzee alicheka na kulia wakati huo huo.


“Mama, samahani.” Jones alibubujikwa na machozi, akijihisi mnyonge. “Nilitiwa moyo na wawili hao, mama na bintiye. Sikutaka kukukuua, samahani. Tafadhali niache uende…”


"Kwa kuwa unajua kuwa ulikosea, nitakuondoa sasa." Mkono wa mwanamke mzee ulimshika, lakini Jones aliogopa sana kusogea. Doa lenye unyevunyevu lilimtoka kwenye ‘gongo’ lake huku akijikojolea. Taa ziliwaka ghafla!


Maafisa kadhaa wa polisi walitoka jikoni, na mwanamke mzee kwenye kiti cha magurudumu akavua wigi lake kabla ya kusimama.

Jones alipigwa na butwaa na kutetemeka. “Shangazi Manka…”


"Bwana. Jones, kuna mtu aliripoti kwamba unashukiwa kumuua Madam Bibi Masawe. Na wewe mwenyewe umekiri hapa. Polisi sasa wanakukamata rasmi.” Afisa huyo akatoa pingu na kumfunga mikono.


“Hapana, hapana…” Jones alijitahidi sana kujificha. “Nilikunywa pombe kupita kiasi. Nilikuwa naongea ujinga tu.”


"Mjomba, nimerekodi kila neno ulilosema." Lisa alitoka na simu. Uso wake ulikuwa umejaa huzuni. “Ulikuwa mwana pekee wa kiume wa bibi. Alikuwa mzuri kwako na alikulea kwa uchungu, lakini mwishowe, ulipanga njama na wengine kumuua. Bado unakumbuka jinsi alivyokufa? Je, huoti ndoto mbaya? Je! dhamiri yako haikuumi?”


“Usiseme tena…” Jones alikuwa tayari amekunywa pombe nyingi. Sambamba na jinsi alivyokuwa amepatwa na woga, akili yake ilikuwa karibu kuzimia.


Lisa alisema kwa ujeuri, “Tayari nimekusanya ushahidi mwingi. Ikiwa hutaki kufa gerezani, bora utoe ukweli wako kwa uaminifu.

Vinginevyo, Mama Masawe bila shaka atajaribu kukwepa mashtaka mahakamani baadaye.”


Jones hakumwamini. “Umekusanya ushahidi gani?”


"Bibi alitibiwa hospitalini, na hospitali ina rekodi zake za matibabu. Daktari alisema kwamba ingawa bibi alikuwa amepooza wakati huo, haikuwezekana afe ghafla hivyo. Pia kuna Aunty Helen ambaye ulimwajiri badala ya Aunty Manka kumtunza Bibi. Yuko tayari kufika mahakamani sasa…”


Jones aligeuka rangi. Alijua kwamba alikuwa katika matatizo.


Kama asingetoa ushahidi muda huo, basi angeweza kuishia jela wakati Mama Masawe angesukuma shutuma hizo kwake. “Sawa, nitakiri. Ilikuwa Mama Masawe. Alichukua fursa wakati bibi yako alikuwa amelala na…” Labda ilikuwa dhamiri yake ya mwisho, lakini hatimaye Jones alianguka chini na kulia.


Lisa na Aunty Manka nao walilia. Hawakutarajia mwisho wa Madam Bibi Masawe kuwa mbaya kiasi hicho.


Aunty Manka aliuliza, “Swali la mwisho. Siku hiyo bibi madam Masawe alipoanguka kutoka kwenye ngazi, ni Lina ndiye aliyemsukuma?"


"Kwa kweli sijui kuhusu hilo." Jones Masawe alitikisa kichwa, lakini akifikiria juu ya utu wa Lina, alihisi kwamba labda alifanya hivyo. Hata hivyo, alikuwa na binti mmoja tu na hakutaka aende jela.


Mwishowe, Jones alichukuliwa na polisi kwa mahojiano. Lisa alitazama jumba la giza nyuma yake. Hapo awali palikuwa nyumbani kwake, lakini sasa palikuwa mahali ambapo hakutaka tena kukanyaga. Alichukua funguo na kuzitupa kwenye nyasi kabla ya kugeuka na kutoka nje ya mlango.


Gari lao la kifahari lilikuwa limeegeshwa mlangoni. Alvin alikuwa amesimama huku kaegemea gari. Kulikuwa na mvua kidogo usiku huo, na matone ya mvua yalitua kwenye kichwa na mabega yake. Lisa alimtazama kwa mahaba, macho yake mazito na safi yalipendeza kama mwanga wa nyota pekee angani.


Wakati huo, Lisa, ambaye hakuwa na nyumba, alionekana kuwa amepata nyumba. Aliruka mikononi mwake, na Alvin akafunua koti lake ili kumfunika ndani yake.


"Alvlisa, hatimaye nimelipiza kisasi." Lisa akasonga mikononi mwake. “Lakini sina furaha hata kidogo. Ninajuta kwamba sikukaa zaidi na Bibi hapo awali. La sivyo, asingekufa vibaya hivyo.”


Machozi ya Lisa yalilowanisha shati kifuani mwa Alvin. Alvin hakujua jinsi ya kuwafariji wengine. Alimsubiri amalize kulia na huku akimpigapiga tu kichwani. “Umefanya vizuri usiku wa leo. Hakukuwa na ushahidi wowote bado uliweza kumfanya Jones Masawe akiri yeye mwenyewe!"


“Nilicheza kamari, kupata ama kukosa. Nilicheza kamari juu ya ubinadamu wake. Nilicheza kamari kwenye kile kilichosalia kwenye hatia na dhamiri ya Jones. Nilicheza kamari kwamba angekuwa mbinafsi kiasi cha kumsingizia Mama Masawe.” Sauti ya Lisa iliendelea kusikika. "Nilikuwa tayari nadhani kwamba Jones asingefanya hivyo mwenyewe. Ili kupunguza adhabu yake, bila shaka angesema kwamba ni Lina au Mama Masawe waliofanya hivyo. Kwa kweli sikutarajia Mama Masawe angekuwa mkatili kiasi hicho.”


“Mama Masawe ana uhakika wa kwenda jela. Twende, usiku umeenda sana.” Alvin alifungua mlango wa gari.


Lisa ghafla akashika mkono wake. Macho yake makubwa meusi yalitazama ndani yake aliposema, “Alvlisa, nina wewe tu sasa. Utaniacha pia?”


“Sitafanya hivyo.” Alvin akainama na kumbusu kwenye paji la uso huku akiongea kwa upole.


Lisa alifumba macho. Kwa wakati huo, alifikiria kwamba asingemuacha kamwe maishani mwake. Ni baadaye tu ndipo alipogundua kwamba walikuwa bado wachanga sana kwenye mapenzi, na kulikuwa na mambo ambayo yangebadilika.

•••

Saa tisa usiku, Lina na Mama yake walikuwa wamelala fofofo kwenye chumba cha hoteli. Kengele ya mlango ililia ghafla.


"Ni nani huyo?" Mama Masawe alifungua mlango kwa hasira. Alifikiri kwamba ni Jones ndiye aliyewafuata kuwafanyia fujo.

Hata hivyo, mara mlango ulipofunguliwa, kundi la polisi liliingia na kumfunga pingu. “Mama Masawe, unashukiwa kumuua Mzee Madam Masawe. Upo chini ya ulinzi!”


"Nini?" Mama Masawe alipigwa na butwaa na kuruka kwa haraka. "Sikumuua mimi."


“Mumeo tayari ameshatoa maelezo kamili kituoni. Ni wewe uliyemkaba mama mkwe wako kwa mikono yako mwenyewe.” Macho ya polisi yalijaa dharau. Mwanamke huyo hata alimuua mama mkwe wake mwenyewe! Mtu wa aina hii hakuwa na maadili kabisa. Polisi hawakumpa nafasi ya kujitetea, wakamtoa nje.


“Mama, nini kinaendelea?” Lina alikurupuka kutoka kitandani na kukimbilia kumshika, lakini polisi hawakumruhusu kumgusa.


Sura ya 133


Mama Masawe akapaza sauti na kusema, “Baba yako ni mnyama! Kaenda kunichongea polisi kuwa nilimuua bibi yako. Lina, lazima ujilinde.”


Mama Masawe alichukuliwa upesi, na Lina akaanguka chini. Alikuwa ameteseka kijijini kwa zaidi ya miaka 20, na haikuwa rahisi kwake kuja mjini. Lakini, kabla hata mwaka haujaisha, familia yake ilisambaratika kabisa! Ikiwa kitu kingetokea kwa Jones Masawe na Mama Masawe, angekuwa na sifa gani za kuwa binti mkubwa wa familia ya Jones? Hapana, hapana. Hakutaka kurudi enzi hizo!


Alimpigia simu Stephen Kileo kwa haraka. “Stephen, nakuomba. Tafadhali nisaidie. Mama na baba yangu wamekamatwa na polisi. Maadamu utanisaidia, nakuahidi kuwa nitakuwa mkeo. Nitakupa nusu ya hisa za Mawenzi Investments.”


“Lina Jones, nimeelewa sasa. Bahati mbaya humwandama yule aliye pamoja nawe. Kwanza, ilikuwa Ethan Lowe, na sasa mama na baba yako wanaenda jela. Sifa yangu pia iliharibiwa kabisa na wewe. Potea na ukae mbali nami siku zijazo. Kukuona tu kunanifanya nitamani kutapika!” Stephen alikata simu moja kwa moja.


Lina alipigwa na butwaa kabisa. Hakuweza kuelewa. Haikuwa kitambo kirefu matajiri wote huko Masaki walikuwa wamemshikilia. Ilikuwa imechukua muda mfupi tu, na sasa, kila kitu kilikuwa kimebadilika. Kila kitu kilikuwa kosa la Lisa Jones! Aliamini ni Lisa aliyemharibia maisha na kumdumbukiza katika hali hiyo mbaya. Kwa nini Lisa alikuwa bado yupo hai?! Moyo wa Lina ulikuwa umejaa wazimu.


Wakati huo alikumbuka kitu kama mtu aliyeshukiwa na roho mtakatifu na kufunuliwa jambo. Alikumbuka alikuwa na picha za Lisa alizopigwa hotelini siku ambayo Lina alimtengenezea njama za kubakwa. Ni siku ile ambayo alilaghaiwa kwenda kuwasilisha michoro yake hotelini kwa ajili ya mradi wa Mawenzi aliokuwa akiupigania kuupata, ambapo kwa bahati nzuri aliokolewa na Kelvin. Alikumbuka picha hizo zilikuwa kwenye simu yake. Alipoziona, alishtuka kwanza kabla ya kusisimka mara moja.


Picha hizo zilikuwa za Lisa akiwa karibu sana na Kelvin Mushi utasema ni wapenzi. Alijua kutoka eneo ambalo picha zilipigwa kuwa ni wakati wa kumtia Lisa dawa ndani ya chumba cha hoteli.


Hapo awali, Lina alitaka wanaume fulani wambake Lisa, lakini Kelvin Mushi alikuwa amefika kwa wakati. Lakini Lina alifanikiwa kupata picha za video zilizomwonyesha Kelvin akiwa kamnyanyua Lisa mikononi mwake. Hakutarajia kamwe kwamba zingekuwa bado zimo kwenye simu yake.


“Haha, kwa picha hizi, Lisa atawezaje kukaa na Alvin?” Lina aliwaza kwa furaha. Sifa yake kama mwenyekiti wa Mawenzi Investments pia ingeathiriwa. Lina alitafuta haraka nambari ya mwandishi wa udaku!

•••

Saa tatu asubuhi Lisa alipoamka, alikuwa peke yake kitandani. Mvua ilikuwa imenyesha usiku kucha na alilala usingizi mnono sana. Sasa kwa kuwa alikwisha lipiza kisasi kwa kifo cha bibi yake na Bibi na Bwana Masawe wote walikuwa jela, alihisi utulivu na raha kwa mara ya kwanza baada ya muda mrefu. Pia ilikuwa ni nadra kwake kuamka akiwa amechelewa sana.


Alikaa na kuangalia muda lakini akagundua kuwa kuna missed call nyingi kwenye simu yake. Nyingine zilikuwa kutoka ofisini, nyingine kutoka kwa Kelvin, na hata kulikuwa na missed calls nyingi zaidi kutoka Pamela. Pamela alikuwa amempigia simu mara saba au nane.

Haraka alimpigia tena huku akicheka. “Mbona umenipigia simu mara nyingi sana asubuhi? Kuna kitu kilitokea?"

“Kuna kitu kilikutokea? Inamaana bado hujui?” Sauti ya wasiwasi ya Pamela ilisikika. "Nenda uangalie habari zinazovuma sasa."


Lisa alipigwa na butwaa alipoingia mtandaoni. Aliona video iliyokuwa inatrend ikiwa na jina lake na Kelvin na kubofya habari ile. Matokeo ya utafutaji yakasomeka, 'Mwenyekiti mrembo wa Mawenzi Investments afumwa kwenye pozi tata na mpenzi wake' ghafla yalitokea.


Lisa alihisi kuogopa. Alipobofya kwenye makala hiyo, alipigwa na butwaa kuona video ya Kelvin Mushi akiwa kambeba juujuu huku akiwa kamwinamia kama anambusu shingoni. Chumba kilikuwa na baridi, lakini ghafla alihisi joto sana!


“Unafanyiwa njama?” Pamela alisema kwa wasiwasi, "Kwa utu wako, haiwezekani kuwa na uhusiano wa kimapenzi na mtu mwingine zaidi ya Alvin. Ninakuamini, lakini wengine wanaweza wasikuamini.”


Pamela alikuwa hajamaliza kuongea wakati mlango wa chumba cha kulala ulifunguliwa kwa nguvu. Alvin aliingia kwa nguvu huku uso wake mzuri ukiwa umefunikwa na hasira kali. Machoni mwake kulikuwa na sura iliyoonyesha hakutaka kitu zaidi ya kumrarua vipande vipande. Lisa alikuwa hajamwona akiwa na hasira hivi kwa muda mrefu. Haraka akakata simu na kumueleza. “Umeona hizo picha? Usielewe vibaya—”


“Kwa hiyo unataka nikupongeze, sivyo?" Alvin aliikamata simu iliyokuwa mikononi mwake na kumrushia. Macho yake ya giza yalifunikwa na tamaa, karaha, na chuki. “Angalia wewe mwenyewe hizo picha za kuchukiza. Unadai kuwa humpendi Kelvin Mushi, lakini ulimkumbatia kwa nguvu na hata kumvua nguo. Lisa Jones, mbona huna haya?”


Simu yake iligonga kifua chake kwa nguvu. Ilimuuma, lakini sio kama moyo wake ulivyouma. Ni wanaume wangapi wangeweza kutulia ikiwa wangeona picha kama zile? Alikuwa kavurugwa kabisa na hizo picha zake.


“Hapana, nilifanyiwa njama, sema tu sikukuambia ukweli! Usiku huo, Lina Jones alinilazimisha kunywa dawa, na Kelvin Mushi alitokea kwa bahati nzuri akaniokoa. Hakuna kilichotokea kati yetu." Lisa alitikisa kichwa kwa masikitiko huku akieleza, “Nilijiloweka kwenye maji baridi usiku kucha.”


"Unanichukulia kama mjinga?" Kicheko cha kutisha cha kijeuri kilisikika kutoka kwenye koo la Alvin. “Uliponilisha kwa hila madawa kama hayo, hata mwanamume kama mimi nilishindwa kuvumilia. Ilinibidi niende hospitalini kuwekewa dripu ili nipate nafuu, lakini wewe unasema ulishinda kwa kujiloweka kwenye maji baridi tu?”


“Ninasema ukweli.” Lisa alilazimisha kujibu malalamiko yake na kujaribu kueleza, “Naweza kuapa—”


"Nyamaza! Lisa Jones, kwa kweli sitakuelewa!” Alvin ghafla akashika kidevu chake kwa nguvu. “Unajifanya kuwa msafi na mtulivu mbele yangu, ukisema kwamba unaogopa… Kumbe ni janja janja yako tu kuendelea kunifanya mjinga?! Ngoja nikuulize. Picha hizi zilipigwa lini? Nakumbuka… nilienda Nairobi kwa siku chache na Shangazi Linda akasema hukurudi usiku kucha…”


“Sikufanya hivyo! Hakuna kilichotokea kati yangu na Kelvin, simpendi…” Lisa akatikisa kichwa kwa nguvu.


"Kwa hivyo mawazo yangu yalikuwa sawa." Alvin hakumsikiliza hata kidogo. Macho yake yalijaa dhihaka na kejeli. “Nilikupigia simu usiku ule. Simu yako ilikuwa imezimwa usiku kucha. Hah, kumbe ulikuwa na Kelvin Mushi, sivyo?"


Kadri alivyozidi kuongea ndivyo hasira zilivyozidi kumpanda. Ilikuwa ni kama kuna jeraha kwenye moyo wake, na chumvi iliendelea kupakwa juu yake. Ilimuuma sana hata akashindwa kupumua.


Pamoja na mashaka na shutuma zake, moyo wa Lisa ukazidi kuwa mzito na mzito. Kulikuwa na uaminifu mdogo sana kati yao. Kwa kweli hakujua jinsi ya kumshawishi. “Kama… Kama huniamini, unaweza kuangalia mwenyewe,” Lisa alikunja ngumi na kusema bila kujielewa.


Alvin alicheka kana kwamba amesikia mzaha. Sauti yake ilijaa dharau alipozungumza, “Baada ya kutazama hizo picha, kukutazama tu kunanifanya nijisikie mchafu. Sitathubutu kushika mwili wako mchafu. Kumbe ndiyo maana jana machale yalishika nikaacha.”


Lisa alijeruhiwa sana moyoni mwake. Jana yake usiku, alijisikia kana kwamba alikuwa mwanamke mwenye furaha zaidi duniani, lakini mara tu kulipopambazuka, ilionekana kana kwamba dunia nzima ilikuwa imeporomoka. Picha hizo zilitoka wapi? Alikumbuka kwamba wakati wanaondoka, Kelvin alisema kwamba aliivunja kamera. Haraka akapiga namba ya Kelvin.


Simu ilipounganishwa, sauti ya Kelvin ya wasiwasi ilisikika. “Lisa, tayari nimeshaona kila kitu. Mimi sina neno ila nina wasiwasi na wewe. Alvin atakuelewa kweli? Naweza kumpigia simu ili nimweleweshe?”......ITAENDELEA.....

Unafikiri nini kitafuata hapo maana mambo ni moto mambo ni fire, lakini sina cha kusema nikuombe tuungane pamoja katika sehemu inayofuata ya mkasa huu wa kusisimua unaokwenda kwa jina la LISA.